Home

TUZO YA KISWAHILI YA SAFAL-CORNELL

YA FASIHI YA AFRIKA

 Tangazo la Washindi wa 2023

Washindi wa Tuzo ya Kiswahili ya Safal-Cornell ya Fasihi ya Afrika kwa mwaka 2023 walituzwa na Dkt. Caroline Asiimwe, Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki (EAKC) kwenye hafla maalumu iliyofanyika Februari 9, 2024, kwenye Hoteli ya Movenpick, Nairobi.

Tuzo hii inafadhiliwa na kampuni ya Safal Group, kupitia matawi yake ya Mabati Rolling Mills (MRM), Kenya na ALAF, Tanzania; Kituo cha Taaluma za Afrika cha Chuo Kikuu cha Cornell, Marekani; na Wakfu wa Ngugi wa Thiong’o.

Madhumuni makuu ya Tuzo hii, iliyoanzishwa mwaka 2014 na Dkt. Lizzy Attree na Dkt. Mukoma wa Ngugi (Chuo Kikuu cha Cornell, Marekani), ni kuthamini uandishi kwa lugha za Kiafrika, kuhimiza sanaa ya tafsiri baina ya lugha za Kiafrika zenyewe kwa zenyewe, na pia kutafsiri maandishi ya lugha nyengine kwa lugha za Kiafrika.

Majaji wa mwaka 2023, Prof Kyallo W. Wamitila wa Chuo Kikuu cha Nairobi, Dkt. Zuhura Badru wa Chuo Kikuu cha Dodoma, na Bw. Ali Mwalim Rashid wa Chuo Kikuu cha Taifa, Zanzibar,walichagua mswada wa Dunia Duara ulioandikwa na Philipo Oyaro (Tanzania), kuwa mshindi wa kwanza katika Kitengo cha Riwaya; na mswada Changa la Macho, ulioandikwa na Fatuma Salim (Zanzibar, Tanzania), kuwa mshindi katika kitengo cha Ushairi. Kila mmoja wao alipokea Dola za Marekani 5,000.

Dunia Duara ni riwaya ya kihalifu na kipelelezi inayohusisha mbinu za kisasa katika ufumbuzi, na yenye wahusika wanaoaminika, lugha yenye taswira nzuri na matumizi mazuri ya taharuki.

Dhamira ya ujenzi wa jamii ndiyo inayotawala mashairi ya Fatuma Salim yaliyomo kwenye mswada wake,  Changa la Macho. Mbali na maudhui mazito, mshairi ametumia lugha yenye matumizi ya picha, ishara na tamathali, na yenye athari na ulinganifu mzuri wa fani na maudhui.

Katika hotuba yake, Dkt. Asiimwe aliwapongeza washindi hao na kuupongeza uongozi wa Tuzo ya Safal-Cornell, bodi yake, na wadhamini – wakiongozwa na Safal Group – kwa kazi yao muhimu ya kukuza fasihi katika lugha za Kiafrika, hasa Kiswahili.

Mkurugenzi Mtendaji wa Safal Group, Bw. Anders Lindgren, naye alizungumza katika hafla hiyo na kuangazia umuhimu wa lugha ya Kiswahili katika maendeleo ya ukanda wa Afrika Mashariki. “Kupitia uungwaji mkono wetu wa Tuzo hii, kampuni za Kundi la SAFAL zimejitolea kwa dhati kuendeleza lugha za Kiafrika, na nawapongeza Wakfu wa Safal-MRM kwa kazi yao ya kuandaa sherehe hizi za Tuzo.”

Kwa niaba ya majaji wenzake, Mwenyekiti wa Jopo la Majaji, Prof Wamitila, aliwapongeza washiriki wa mwaka 2023 kwa uandishi wao wa hali ya juu, kiasi cha kwamba ilikuwa vigumu kwa majaji kuchagua washindi wa kwanza. “Huu ni ushahidi tosha kwamba tuna hazina kubwa ya ubunifu, hasa miongoni mwa vijana, unaovuka mipaka ya kila nchi, na ambao utaimarisha uandishi na uchapishaji wa Fasihi ya Kiswahili,” aliongeza Prof Wamitila.

Mshindi wa pili katika Kitengo cha Riwaya alikuwa ni Ahmad Simba (Tanzania) aliyeandika Safari ya Maisha; na mshindi wa pili katika kitengo cha Ushairi alikuwa ni Lenard Mtesigwa (Tanzania) kwa diwani yake itwaayo Ndani ya Subira Kichwangomba. Kila mmoja alitunukiwa Dola za Marekani 2,500. Wote wawili walikuwa wameorodheshwa kwenye Orodha Fupi ya mwaka 2022.

Safari ya Maisha ni hadithi ya usimulizi wa kuvutia, na inamfunulia msomaji taswira za maisha ya kisasa na changamoto zake, kama vile mivutano na mashindano ya kifamilia, uhalifu na ubaguzi wa rangi.

Majaji walisema pia kuwa diwani ya Ndani ya Subira Kichwangomba imetia fora kwa sababu ya maumbo na miundo tafauti iliyotumika, lugha ya kitamathali na toni inayoshabihiana vyema na mada mbalimbali zinazojadiliwa.

Kama ilivyotangazwa awali, miswada mengine iliyoteuliwa ilikuwa ni: Salome Anaishi,  riwaya iliyoandikwa na Nicholas Ogal, na diwani Maisha ya Kesho,  mashairi yaliyoandkwa na John Karithi – wote wawili kutoka Kenya.

Mikusanyo miwili ya hadithi fupi pia iliorodheshwa. Nayo ni Mtoto wa Mama na Hadithi Nyingine, wa Edwin Omindo (Kenya), na Koti la Karani na Hadithi Nyingine, wa Stallone Joyfully (Tanzania).

Washindi hao na wenzao walikuwemo katika Orodha Fupi pia walihudhuria hafla hiyo ya utoaji tuzo jijini Nairobi.

Kwa Wahariri: 

Tuzo ya Kiswahili ya Safal-Cornell ya Fasihi ya Afrika, yenye thamani ya jumla ya Dola za Marekani 15,000, hutolewa kila mwaka kwa miswada bora katika fani za riwaya, ushairi, wasifu, tamthilia na riwaya za picha. Miswada inayoshinda huchapishwa vitabu na shirika la Mkuki na Nyota. Na mswada bora wa ushairi hufasiriwa kwa Kiingereza na kuchapishwa kitabu na shirika la Africa Poetry Book Fund.

Tuzo hii inadhaminiwa na kampuni ya Mabati Rolling Mills, Kenya, na kampuni ya ALAF Limited, Tanzania (ambazo ni miongoni mwa kampuni za Safal Mauritius Limited); pia na Ofisi ya Makamu wa Mkuu wa Maswala ya Kimataifa katika Chuo Kikuu cha Cornell, Idara ya Taaluma za Afrika ya Chuo Kikuu cha Cornell, Marekani; na Wakfu wa Ngugi wa Thiong’o (Ngugi wa Thiong’o Foundation).

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Kampuni ya Safal Investments Mauritius Limited na matawi yake (ambayo ni pamoja na Mabati Rolling Mills Limited, Kenya, na ALAF Limited, Tanzania) inajulikana kwa jina la jumla la The Safal Group. Hii ni kampuni kubwa kabisa inayotengeneza mabati katika nchi 12 za Afrika. www.safalgroup.com

Mabati Rolling Mills Limited (MRM) ilibuniwa zaidi ya miaka 50 iliyopita. Ni kampuni kubwa kabisa Kenya inayotengeneza mabati ya kuezekea mapaa, na inaongoza katika utanzu huu wa ufundi. Pia inaongoza katika bara la Afrika kwa kutengeneza mabati ikitumia teknolojia ya hali ya juu kabisa inayopatikana duniani. Mabati yake maarufu yanasifika na yanaaminiwa na mamilioni ya wajenzi. www.mabati.com

Safal MRM Foundation, yenye makao yake Kenya, ni kitengo cha Mabati Rolling Mills na Safal Group kinachoshughulika na kutoa misaada ya aina mbalimbali. Miongoni mwa misaada hiyo, inayotolewa Mariakani, Kenya, ni kuanzisha na kuendelea kugharimia uendeshaji wa Taasisi ya Mabati ya Mafunzo ya Teknolojia (Mabati Technical Training Institute), na Kituo cha Mabati cha Matibabu (Mabati Medical Centre). www.safalmrmfoundation.org

ALAF Limited (ALAF) ni kampuni ya Tanzania inayoongoza katika utengenezaji wa mabati ya kuezekea mapaa. Tangu ilipobuniwa mwaka 1960, ALAF imeendelea kuchangia kwa kiasi kikubwa katika shughuli za ujenzi nchini. ALAF haitengenezi mabati ya kuezekea mapaa tu, bali pia aina za nyaya za chuma zinazotumika katika ujenzi wa mapaa. ALAF pia inatengeneza mabomba ya metali yanayotumika katika shughuli mbalimbali za ufundi. www.alaf.co.tz

Ofisi ya Makamu wa Mkuu wa Maswala ya Kimataifa katika Chuo Kikuu cha Cornell inatoa mwongozo na kusaidia katika kusimamia juhudi za kuzidisha shughuli za kimataifa Cornell. Lengo lake ni kushirikiana na shule, vyuo na taasisi nyengine ili kuendeleza na kutekeleza mipango inayohusiana na shughuli za kimataifa za Chuo Kikuu hiki. Ofisi hii inaisaidia Halmashauri mpya ya Kimataifa, ambayo mwenyekiti wake ni Makamu wa Mkuu. http://international.cornell.edu/international_vision

Idara ya Taaluma za Afrika na Utafiti inachangia kwa kiasi kikubwa katika shughuli za kitaaluma, kitamaduni na za kijamii kwenye Chuo Kikuu cha Cornell, Ithaca. http://africana.cornell.edu

Ngugi Wa Thiong’o Foundation.Wakfu huu unapata nguvu zake kutokana na hamu na ari ya kukuza na kuonekana kwa Lugha za Kiafrika nchini Kenya, barani Afrika, na duniani, na kutambuliwa kuwa ni vyombo mwafaka vya kuendeshea shughuli za sanaa ya uigizaji, ubunifu, uvumbuzi, na taaluma. Pia unazitambua lugha hizi kwamba zina uwezo wa kuwa mstari wa mbele katika kila fani – tangu utamaduni, sayansi za kibiolojia, teknolojia hadi tiba.   http://ngugiwathiongofoundation.org

Mkuki na Nyota Publishers ni shirika huru la uchapishaji vitabu vya kimaendeleo, kiukombozi, vya bei nafuu na maridadi. Shirika hili lilianzishwa mwaka 1991 kutokana na ukosefu wa vitabu vya kiwango cha juu nchini Tanzania. Kaulimbiu yake ni kuchapisha “Vitabu Vinavyofaa, Vitabu vya Bei Nafuu, na Vitabu Maridadi. http://www.mkukinanyota.com

Africa Poetry Book Fund inaimarisha na kuendeleza uchapishaji wa sanaa za kishairi kupitia vitabu vyake, mashindano, warsha, semina, pamoja na kushirikiana na wachapishaji, matamasha, mawakala, vyuo, vyuo vikuu, makongamano, na vikundi vyengine vinavyohusika na ushairi Afrika. http://africanpoetrybf.unl.edu/

Bodi ya Wadhamini: Abdilatif Abdalla (Mwenyekiti), Mukoma Wa Ngugi, Lizzy Attree, Walter Bgoya, Henry Chakava, Chege Githiora, Clarissa Vierke, Farouk Topan, Carole Boyce Davies, and Ngugi Wa Thiong’o.

Mkurugenzi: Munyao Kilolo

Tovuti: http://blogs.cornell.edu/kiswahiliprize/

Twitter: @KiswahiliPrize

Facebook: https://www.facebook.com/pages/Mabati-Cornell-Kiswahili-Prize for

African-Literature/1534905843433822

Mawasiliano: Prof. Mukoma Wa Ngugi, Cornell University, kiswahiliprize@cornell.edu Dr Lizzy Attree, kiswahiliprize@cornell.edu, Moses Kilolo  kiswahiliprize@cornell.edu.

 

 

Skip to toolbar